Na Bakari Mwakangwale
VIONGOZI wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) wametakiwa kuweka mbele maslahi ya jamii ya Waislamu, huku vipaumbele vyao vikiwa ni kusimamia masuala ya uchumi na elimu.
Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa BAKWATA Taifa, Alhaj Nuhu Jabir Mruma, Jumapili ya wiki iliyopita Jijini Dar es Salaam, akikumbusha wajibu wa viongozi wa Baraza kwa umma wa Kiislamu.
Alhaj Mruma alisema kwa kuwa uchaguzi Mkuu umekamilika na viongozi waliomba kuchaguliwa wamechaguliwa sasa kinachotakiwa kwao ni kufanya kazi ya kuwatumikia Waislamu.
Alhaj Mruma, amewakumbusha viongozi hao kuwa katika muda wao wa uongozi waweke mbele maslahi ya jamii ya Waislamu, akikazia masuala ya Uchimi na Elimu.
Aidha, akawataka viongozi hao wa ngazi za juu wa Bakwata, wakiwemo Masheikh, Wenyeviti na Makatibu pamoja na Mabaraza ya Masheikh na Halmashauri za Mikoa, Wilaya na Kata kufanya kazi kwa pamoja na kwa uwazi kama timu yenye mlengo mmoja.
“Siyo sawa kwa Sheikh, Mwenyekiti, Katibu wa Mkoa au ngazi nyingine kufanya kazi na kuamua jambo peke yake hali hiyo inaleta au kukaribisha migogoro ni lazima tuzingatie umuhimu wa uongozi, mipango na maamuzi shirikishi.” Amesema Alhaj Mruma.
Ili kuepusha migogoro akawataka viongozi wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) kuisoma, kuiheshimu na kufuata Katiba ya BAKWATA.
Alhaj Mruma, amesema kuna umuhimu kwa viongozi na maafisa wakongwe kuheshimu Katiba ama kwa viongozi wapya ni muhimu kuisoma, kuielewa na kuifuata katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
“Jambo muhimu ni kuzingatia katiba na taratibu zingine pamoja na kanuni wakati wa utendaji, viongozi waheshimiane na wale wa ngazi moja washirikiane kikamilifu kwa kufanya hivyo kutaleta tija kwa jamii ya Waislamu na kinyume chake ni sawa na kukaribisha mdororo wa uongozi na umma kwa ujumla.” Amesema.
Amesema, jambo lolote linapojitokeza lenye kuashiria kuvuruga umoja na mshikamano lishughulikiwe haraka na ngazi husika, akasema pasitokee viongozi kuvusha jambo hadi ngazi za juu pasi na sababu za msingi.