Kupokelewa kwa Shangwe Zanzibar iwapo…
Watu wasipupie dunia, wazingatie “Barzakh”
Na Mwandishi Wetu
Ismail Jussa Ladhu amegusa nyoyo za watu wa Donge, alipoanza hotuba yake kwa kupaza sauti juu ya kadhia ya Sheikh Mselem na Masheikh wenzake kushikiliwa kwa muda mrefu bila ya kuhukumiwa.
Jussa katika hotuba yake ya kampeni mapema wiki hii, amesema kwamba, anaona kitendo hicho ni dhulma na hivyo kuziomba mamlaka husika kuzingatia haki na uhuru wa Masheikh hao.
Akiwahutubia wananchi wa Mahonda na Donge katika Uwanja wa Mwanakombo, Jussa amesema kwamba si jambo jema Masheikh wenye kuheshimika kutendewa isivyo haki, bali ni dhulma inayostahiki kupingwa.
Akasema, iwapo Chama chake cha ACT-Wazalendo kitafanikiwa kuchukua serikali ya Zanzibar, basi jambo la mwanzo itakuwa kuhakikisha kwamba Sheikh Mselem Ali, kijana wa Donge, na wenzake wanaachiwa na kwamba watapokelewa Unguja kwa shangwe.
Katika nasaha zake kwa watu Unguja Kaskazini na Zanzibar kwa ujumla akasema kwamba, ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha kwamba hasaidii kwa namna yoyote kuendeleza au kuunga mkono dhulma wanayofanyiwa Masheikh.
Akasema, kila anayesadia dhulma hii kwa namna yoyote, basi ajiandae kujibu maswali mbele ya Mwenyezi Mungu kwani, mafundisho ya Dini yanataka watu sio tu wajitenge na dhulma, lakini pia waikemee. Na kwamba kukemea dhulma ni katika ucha-Mungu.
Katika nasaha zake za ujumla, Jussa aliwaelekea wanasiasa akiwaasa, wasiangalie tu manufaa ya dunia, lakini watazame na kujiuliza hali itakavyokuwa wakiwa katika “Mwanandani” kaburini katika maisha ya “Barzakh”.