Saudia yaanza kupokea maombi ya Umrah
Saudi Arabia kupitia Wizara ya Hija na Umrah imetangaza kuwa kuanzia Jumatatu, wiki hii itakubali maombi ya kutekeleza Ibada ya Hija ndogo ya Umrah kutoka nje ya nchi ambapo kunatarajiwa kutapokelewa watu wapatao milioni mbili.
Kulingana na habari hiyo katika shirika rasmi la habari la Saudi Arabia SPA, Naibu Waziri wa Saudi Arabia wa Hajj na Umrah, Abdulfettah Bin Süleyman, amesema kuwa Masjid al-Haram, ambayo pia inajumuisha Kaaba, iko tayari kukaribisha Umrah na waumini kutoka nchi za nje.
Bin Suleiman, amebaini kuwa kwa kufuata hatua za kupambana na janga la corona, watu 60,000 watakubaliwa kila siku na takriban milioni mbili kwa mwezi.
Kwa wenyeji na wakazi, chanjo ya COVID-19 ni sharti la kutekeleza Umrah na kutembelea na kusali katika Misikiti miwili mitakatifu ya Makah na Madina. Wanaotoka nje ya Ufalme wa Saudia ni lazima wawasilishe cheti rasmi cha chanjo kutoka nchi zao, pamoja na chanjo hiyo kutoka kwa orodha ya chanjo zilizoidhinishwa na Saudi Arabia. Wanaowasili Saudia pia wanapaswa kuzingatia taratibu za karantini.
Naibu waziri alisema kuwa idadi ya abiria kwenye chombo cha kusafirishia haitazidi asilimia 50 ya uwezo wake, huku wasafiri wakitakiwa kutokaribiana.
Bin Suleiman amesema kuwa Wizara inafanya kazi kwa uratibu na mamlaka, ili kujua nchi ambazo watu wa Umrah watakubaliwa na kuamua idadi yao.
Akibainisha kuwa chanjo zilizoidhinishwa za Kovid-19 huko Saudi Arabia ni sharti la kutekeleza Umrah na kuswali huko Masjid al-Haram na Masjid an-Nabawi, Bin Suleiman, alisisitiza kuwa Mahujaji wa Umrah kutoka nje wanapaswa kuwa na nyaraka zao zinazoonyesha kwamba wamepewa chanjo .trt.net.tr/ (IQNA).