Na Omar Msangi
Ilikuwa ni John Forbes Kerry, ambaye kwa mara ya kwanza alifichua hadharani kwamba upo mpango wa kuigawa Syria katika vinchi vidogo vidogo vinavyohasimiana (Tazama: Kerry: If Ceasefire Fails, Partition of Syria is ‘Plan B’)
Akiongea katika Kamati ya Seneti ya Mambo ya Nje (Senate Foreign Relations Committee) mwaka 2016, wakati huo akiwa ‘Secretary of State’, John Kerry alisema kuwa suluhisho la vita Syria ni “Plan B”.
Japo Kerry hakufafanua zaidi katika kikao hicho, lakini ‘Plan B’ aliyomaanisha ni kuigawa Syria katika mapande ya vinchi vidogo vidogo vyenye kuhasimiana, ikiwemo ‘Himaya ya ISIS’ au ‘ISIS Caliphate’ (Salafi), ambayo ni Suni katika eneo la Aleppo, wakipakana na Suni wengine katika Damascus, hawa wakiwa mahasimu wao kwa wao kama ilivyo sasa katika vita.
“Plan B” (de facto Balkanizing Syria) ya Waziri wa Mambo ya Nje, John Forbes Kerry, ilibuniwa toka mwaka 1982 kama ilivyokuwa imeelezwa na mwandishi wa Kiyahudi Oded Yinon katika makala yake aliyoipa jina: "A Strategy for Israel in the Nineteen Eighties."
Yinon aliandika makala hiyo akichambua mipango na mikakati ya Kizayuni Mashariki ya Kati- The Zionist Plan for the Middle East ikilienga kuzisambaratisha nchi za Waarabu (Waislamu) kusiwe na nchi yenye nguvu za kuitishia Israel. Kama alivyowahi kusema Condoleezza Rice, mkakati huo kwa msamiati mwingine hutajwa kama: "Project For a New Middle East." Mwaka 2006 kiasi miaka mitano kabla hata ya kuanza vita ya Syria, aliyekuwa Balozi wa Marekani katika Syria, William Roebuck, alitoa taarifa White House akieleza kuwa ulikuwa wakati muafaka kuchochea chuki, uhasama na machafuko baina ya Sunni na Shia wa Syria ili kuandaa mazingira ya kumpindua Rais Bashar Assad. Na wakati wapiganaji wa ‘Kisalafi’ (Salafist insurgency) walipokuwa wakipata nguvu mwaka 2012, mshauri wa siasa (political aide) wa Hillary Clinton, Bwana Sidney Blumenthal alimtumia ujumbe akimwambia:
"Kuanguka utawala wa Assad kutachochea uhasama na vurugu baina ya Sunni na Shia, na hii itakuwa ni kwa manufaa ya Israel na washirika wake wa Ulaya.”
Kwa bahati mbaya kabisa, katika ulimwengu wa Sunni, vita ya Syria, ndivyo inavyotazamwa. Kuwa ni ugomvi wa Shia na Sunni. Israel wala mabeberu hawaonekani.
Decemba 2012, miezi mitano baada ya kupewa ujumbe huo, Clinton naye akazungumzia vita hiyo akisema kuwa: "Namna bora kabisa ya kuisaidia Israel ni kusaidia harakati za kumpindua Bashar Assad.”
Amerika ilipoivamia Iraq mwaka 2003, lengo ni kuisambaratisha nchi hiyo (Balkanization of Iraq). Kuwe na nchi tatu: Iraq ya Wasuni, Iraq Shia na ya Kurdi, kinyume na ilivyokuwa wakati wa Saddam Hussein, kwamba ilikuwa nchi moja Iraq madhubuti.
Mpango huo huo mchafu, ndio unaelekezwa pia kwa Syria. Hilo aliwahi kulisema Profesa Michel Chossudovsky, Juni 2012 katika Makala yake:
“Hidden US-Israeli Military Agenda: "Break Syria into Pieces." Likasemwa pia katika uchambuzi wa Patrick Henningsen, tarehe 11 Julai, 2012 katika Makala yake: “Syria: The Globalist Destruction of a Nation State.” Hilo litafikiwaje? Katika uchambuzi wake
Professor Michel Chossudovsky, anasema kuwa vitaundwa vikundi vya kigaidi vikipewa majina ya kidini na hivi vitakuwa vikifanya mauwaji ikisingiziwa ama ni Sunni au Shia wamefanya. Na hiyo itakuwa ni njia ya uhakika ya kuchochea uhasama baina ya makundi hayo mawili. Na kwamba, ukisikia Al Qaidah, ISIS, "Muslim terrorists", ni katika makundi hayo ya kigaidi yaliyoundwa kutimiza agenda ya Kizayuni ya Israel na Marekani kusambaratisha nchi za Waarabu. Na hilo ndio analolisema pia mwanahistoria na mchambuzi wa Kimarekani Webster G. Tarpley. Kwamba, ukisikia Al Qaidah ama ISIS, basi ujue kwamba ni magaidi na wapiganaji wale wale waliokuwa wameundwa na mabeberu kupambana na Mrusi kule Afghanistan.Katika uchambuzi wake: "THE SALVADOR OPTION FOR SYRIA": US-NATO Sponsored Death Squads Integrate "Opposition Forces", -Professor Michel Chossudovsky, anaeleza kuwa, kama ilivyowahi kufanyika kule El Salvador, ndivyo itakavyofanyika Syria.
"The Salvador Option": Is a "terrorist model" of mass killings by US sponsored death squads, ambapo ilipotumika kule El Salvador mwaka 1984-1986 ikisimamiwa na Colonel James Steele, zaidi ya watu 75,000 wasio na hatia waliuliwa. Mmoja wa wahanga wa mauwaji hayo akiwa Askofu Mkuu Óscar Arnulfo Romero y Galdámez. Kosa la Archbishop Óscar Arnulfo Romero, ni kuwa aliungana na wanyonge kupinga uonevu, unyonyaji na ubeberu wa Marekani katika nchi ya El Salvador.
Ufupi wa maneno, “Salvador Option” ni mpango wa mauwaji ambapo huundwa vikundi vya mauwaji na utesaji kuleta machafuko katika nchi. Kwa Syria, Profesa Michel Chossudovsky, anasema ndivyo itakavyofanyika. Ndio ukaona mara tu zilipoanza harakati za ISIS ukaona inatangazwa kuwa wanachinja watu ovyo na kubomoa nyumba za ibada za Mashia hata Sunni (wasio Salafi) wasiofuata mrengo wao.
Ili kuhakikisha kuwa mpango huo unatekelezwa vizuri, John Dimitri Negroponte, aliyetekeleza "Salvador Option for Iraq" mwaka 2004-2005, akachaguliwa kuwa balozi wa Syria Januari 2011, kiasi miezi miwili kabla ya kuibuka machafuko ya kumpindua Bashar Al Assad.
Katika mjadala kabla ya kuidhinishwa na Bunge la Seneti kuwa Balozi Iraq, baadhi ya Maseneta walihoji mantiki ya kumteua Negroponte, mtu ambaye anatuhumiwa kuhusika katika mauwaji ya wananchi wa Honduras na El Salvador miaka ya 1980s akiwa Balozi kule. Ilikuwa ni Seneta Christopher John Dodd (D-Conn.) ambaye alisema kwamba nyaraka za “State Department” na CIA, zinaonyesha kwamba Negroponte alihusika katika kuunda vikundi vya utesaji na mauwaji “death squads” vilivyotesa watu, kufanya ubakaji na mauwaji katika nchi za El Salvador na Honduras. Hiyo ikiwa ni namna ya kupambana na wapinzani waliopachikwa msamiati wa magaidi. Hata hivyo, hoja hiyo haikupewa uzito kwa sababu kuteuliwa kwake ilikuwa ni kwa lengo la kufanya yale yale aliyofanikisha El Salvador. Na ndio maana mbinu hiyo ilipotumika Iraq ikapewa jina la “Salvador Option”.
Kilichotarajiwa ni kuwa ngoma ya mauwaji ya ISIS ikishapigwa sana, chuki ya Sunni na Shia ikakolea, itajengwa hoja kwamba watu hawa hawawezi tena kukaa pamoja. Nchi igawanywe. Na kama alivyosema
Patrick Henningsen, kufanya hivyo sio kwa lengo la kuleta Amani, bali kujenga mazingira ya machafuko ya kudumu na kuwa na ‘viserikali’ vidogo vidogo dhaifu ambavyo itakuwa rahisi kuvitia kwapani.
Ikifikia hapo Israel itakuwa ndio mbabe pekee anayetamba Mashariki ya Kati. Kumbuka:
"A Strategy for Israel in the Nineteen Eighties." Kumbuka pia maneno ya Condoleezza Rice: "Project For a New Middle East."
Sasa ushindi wa Bashar katika vita hii, hapana shaka utavuruga mpango mzima wa kuigawa Syria. Ndio maana unamuona Rais Trump kucharuka akitafuta namna ya kuwahami magaidi wa ISIS waliojichimbia Idbil.