Ni kwa wanasiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu Oktoba, 2020
Na Bakari Mwakangwale
WAGOMBEA wa nafasi za uongozi wa kisisa nchini, wametakiwa kuchukua tahadhari kubwa katika kauli na ushawishi wao kwa wananchi pindi watakapo anza Kampeni za kuomba kura na kunadi sera zao.
Wito na tahadhari hiyo umetolewa na Imam wa Masjid Mtoro, Kariakoo Jijini Dar es Salaam, Sheikh Othman Khamisi, akiwahutubia Waislamu katika Khotuba ya Sala ya Ijumaa ya wiki iliyopita.
Imam Khamisi, ametoa tahadhari hiyo kufuatia joto na vuguvugu la Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani nchini likizidi kupanda ambapo Watanzania wanatarajia kupiga kura kuchagua viongozi wao katika nafasi hizo ifikapo Mwezi Oktoba 28, 2020.
Alisema, hiki ni kipindi ambacho Watanzania wapo katika maandalizi ya kuchagua na kuchaguliwa, wale wanaotaka kuchaguliwa wawe na tahadhari kubwa katika kujinadi kwao, waepukane na kauli ambazo zinaweza kusababisha kutoweka kwa amani ya nchi yetu.
“Tahadhari na angalizo langu ni kwa wote waliotia nia ya kugombea nafasi za kisiasa kuanzia Urais, Ubunge, Udiwani, wasisahau kuwa sisi hatuna pa kukimbilia lazima wachunge kitu kinachoitwa amani wasisababishe washabiki wao kuingia na kufanya chochote kitakacho vuruga amani ya nchi yetu.” Ametanabaisha Imam Khamisi.
Alisema wanachopaswa kuelewa wagembea hao ni kuwa amani iliyopo ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kuliko kuwa Mbunge, Rais, ama Diwani kwani yoyote atakae shinda nafasi hizo hawezi kuongoza au kutawala vizuri ili hali amani imevu rugika.
Shekh Khamis, alisema matokeo ya tafiti nyingi zinaonyesha kuwa sehemu mbalimbali Duniani vurugu zinazo zaa mabalaa mengi mara nyingi chanzo chake huwa ni siasa hususan katika kipindi cha Uchaguzi, kutokana na kauli hatarishi za wagombe.
“Amani ndio zawadi katupa Allah, tunakaa kwa amani kuna wale wanaosema kuwa hii sio amani ni uwoga, ukiwa unaogopa na ukaamua kutulia ukaepuka shari ni vizuri zaidi kwani utakuwa umee pusha kutoweka kwa amani.” Amesema Imamu Khamisi.
Shekh Kahamis, akawataka wananchi ambao ndio wadau na wahanga wa kwanza katika vurugu kujiepusha kushabikia siasa zinazoashiria uvunjifu wa amani kwani amani ikivurugika wanasiasa wanao sababisha vurugu wao hukimbia nchi.