Mwenyekiti wa maridhiano ya CCM na CUF
Maridhiano yaliyoleta utulivu na amani Zanzibar
Na Bakari Mwakangwale
MZEE Hassan Nassor Moyo, amerejea kwa Mola wake huku akiamini kuwa ufunguo wa maendeleo ya Zanzibar ni kuwapo na amani ya kudumu na maelewano baina ya raia wake wote bila ya ubaguzi.
Almaruhum Hassan Nassoro Moyo, amefikwa na umautu Agosti 18, 2020, na kuzikwa siku hiyo hiyo, Fuoni Migombani, Zanzibar. Innaalillaah Wa innaaillahr Raajiuun.
Akimzungumzia Almaruhum Mzee Moyo, mara baada ya kifo chake, nguli wa Historia nchini, Mzee Mohammed Said, amesema Mzee Moyo licha ya kuwa asili yake ni Songea Tanganyika, aliipenda Zanzibar na Wazanzibar, kuliko maslahi mengine.
“Mzee Moyo, aliipenda Zanzibar na aliwapenda Wazanzibari na aliipenda amani ya Zanzibar na maendeleo yake, na aliamini kuwa ufunguo wa maendeleo ya Zanzibar ni kuwapo na amani ya kudumu na maelewano baina ya raia wake wote bila ya ubaguzi, Allah (s.w) amghufurie madhambi yake na amtie peponi.” Amesema Mzee Mohammed.
Mzee Mohammed, alisema Mzee Moyo, amefariki wakati Zanzibar inaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu na hakuna asiyejua nini hutokea katika chaguzi za Zanzibar.
Alisema, licha ya kubeba histori nzito ya kabla na baada ya Mapinduzi ya Zanzibar, pia Mzee Moyo, itakumbukwa kuwa alikuwa Mwenyekiti wa maridhiano ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama Cha Wananchi (CUF), mazungumzo yaliyoleta utulivu Zanzibar.
Hili lilikuwa jambo lililokuwa linatakiwa na kuombwa katika kila dua ya Mzanzibari.
“Zanzibar inaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu hakuna asiyejua nini hutokea katika chaguzi za Zanzibar, kama maridhiano yangekuwapo hivi sasa wengi wangelala usingizi usio na lepe ya hofu na mashaka kila wanapofikiria Uchaguzi.”
“Mazungumzo yale yalileta utulivu Zanzibar na kwa Wazanzibar, hili lilikuwa jambo lililokuwa linatakiwa kuenziwa na kuombewa katika kila dua ya Mzanzibari.” Amesema.
Mzee Mohammed, alisema katika maisha yake Mzee Moyo, alikuwa amekanyaga vidole vya baadhi ya wana ASP, wenzake ndani ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kwani lugha ya kuhoji Muungano haikuwa wanayoipenda wao kuisikia.
Alisema, itakumbukwa siku moja Mzee Moyo alighadhibika mbele ya aliyekuwa Spika wa Bunge la Tanzania, Marehem Mh. Samuel Sita, pale alipoambiwa asihoji Muungano.
Aidha, Mzee Mohammed, alisema Mzee Moyo, alikuwa Mwenyekiti wa mpango wa udhamini wa wanafunzi wa Zanzibar, kutoka Serikali ya Oman, udhamini ambao Serikali ya Oman ilijitolea kuwasomesha vijana wa Kizanzibari, katika Vyuo vikubwa duniani kwa gharama yoyote.
Alisema, hiyo ilikuwa ni ndoto ya kila kijana wa Kizanzibari kuwa ndugu zao walikuwa wamewa fungulia hazina yao kwa kuwasomesha ndugu zao katika vyuo vikubwa vyenye hadhi Ulimwenguni.
“Msaada huu mkubwa kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, hakufika mbali umekufa na kila unae muuliza kimetokea nini hana jibu.”
“Serikali ya Umoja wa Kitaifa, iliyotokea baada ya maridhiano baina ya CCM na CUF, Mzee Moyo akiwa Mwenyekiti wake pia imekufa kama zilivyo kuwa Scholarship za Serikali ya Oman ambazo Mwenyekiti wake na aliyezipokea pale State University of Zanzibar (SUZA) alikuwa Marehemu Mzee Hassan Moyo.” Amesema na kufafanua Mzee Mohammed.
(Soma Makala ya Mohammed Said Uk….)