Group Khairat watoa msaada magereza Handeni, Maweni
Na Bint Ally Ahmed
Baraza Kuu la Wanawake wa Kiislamu Tanzania, kupitia kundi la kina mama la mtandao wa Whatsup lenye anuani ya Groups Khairat, wametoa msaada wa chakula chenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni moja na laki tano (1,500,000) kwa wafungwa na mahabusu wanaotumikia vifungo vyao katika gereza la Handeni na gereza la Maweni Jijini Tanga, mwishoni mwa wiki iliyopita.
Baraza Kuu la Wanawake wa Kiislamu limekuwa linafanya kazi kubwa ya kuwaunganisha wanawake wa Kiislamu nchini, linaloongozwa na Ukht. Fatma Ally Chitapa, ambaye pia ndiye kiongozi wa group hilo, limekuwa likiwaelimisha kina mama juu ya dini yao na dunia pia, lakini pia wamejikita kwenye malezi bora ya Kiislamu kwa kuwa mwanamke ndio msingi na nguzo ya familia.
Ukht. Fatma, amesema kuwa kundi lake la Whatsup linalotokana na Baraza Kuu la Wanawake wa Kiislamu hapa nchini, wamekuwa wakijihusisha na kusadia wahitaji mbalimbali kama vile vituo vya watoto yatima na wale wenye uhitaji maalumu na kutekeleza kazi zake mbalimbali za masuala ya kidini kwa kipindi kirefu.
Ukht. Fatma, ameongeza kuwa wamekabidhi chakula hicho kwa Mkuu wa gereza la Maweni, Revocatus Kessy, mchele kilo 300, mafuta ya kupikia lita 60, sabuni boksi kubwa moja, Misahafu ya Tafsiri pamoja na vitabu mbalimbali vya mafundisho ya dini ya Kiislam.
Baadae walikabidhi chakula hicho kwa Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza Anthony Mbogo, kupitia kwa Mkuu wa Gereza la Handeni
mchele Kilo 200, mafuta ya kupikia lita 40, Sabuni boksi kubwa moja, Misahafu ya Tafsiri pamoja na vitabu mchanganyiko vya mafundisho ya Uislamu.
Aidha wafungwa hao nao walipata fursa ya kutoa neno la shukrani kwa wanawake hao na kujiona ni miongoni mwa watu wanao kumbukwa na jamii ya uraiani.
Group Khairat limekuwa likifanya kazi mbalimbali za kheri kwa kuchangishana kidogo walicho nacho na kukifikisha kwa wahitaji.
Kwa kuzingatia umuhimu wao wa kutoa kile walicho jaaliwa na Mola wao, kikundi hicho kila wanapoona kuna shida au uhitaji eneo fulani, huchangishana pesa na kuzipeleka pale wanapoona kuna uhitaji.
Mkuu wa gereza la Handeni, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza Anthony Mbogo na mahabusu walitoa shukran zao za dhati kwa sadaka hiyo waliyoipokea kutoka kwa kina mama hao.
Alisema wafungwa na mahabusu pamoja na watumishi wenzake wanashukuru kwa kile kilichotolewa kwa ajili ya wafungwa.
Mkuu huyo wa gereza aliomba ushirikinao katika kutatua changamoto nyingine kama hizo.
Kwa upande wa Mkuu wa Magereza Wanawake Maweni, Upendo Kazumba, aliwashukuru kina mama hao kwa moyo wao wa kujali na kutoa walicho nacho kwa ajili ya wahitaji na kuwaomba kutowasahau hata kwa kidogo walicho nacho, kwani kutoa ni moyo na sio utajiri.
Msaidizi wa Kikundi hicho cha wanawake Ukht. Mayasa Sadalla, amesema kikundi kimetoa msaada huo kwa wafungwa wa gereza la Handeni na Maweni, Tanga kwa kuona kuwa wana jukumu la kuwakumbuka ndugu zao, hasa wathirika wa kesi za ugaidi wanaoshikiliwa mahabusu kwa muda mrefu sasa.
Ukht. Mayasa, amesema kuwa Baraza la Wanawake wa Kiislamu kupitia group la Khairat, waliguswa na kuona wana wajibu kufanya kila namna kuwasaidia wafungwa kwa kutoa walicho nacho, kwani kutoa ni moyo na kwa Allah hakuna kidogo.
Naye Ukht Fatma, amewaomba Waislamu kulikumbuka kundi hili la watu walioko magerezani, kwani wao wamesahaulika sana na jamii.
Kama una sadaka yako iwe ni magodoro, nguo za wanaume na wanawake, sabuni, mafuta kula, vitabu vya dini ya Kiislamu na mahitaji mengine muhimu ya mwanadamu na unahitaji kuifikisha kwa makundi mbali mbali yanayohitaji, unaweza kuwapigia kina mama hao wanao jishughulisha na mambo mbalimbali ya kheri katika jamii.
Wasiliana na Ukht. Fatma kwa namba hii 0712 326 612.