Saudia yatangaza kanuni za kiafya kwa watakaotekeleza ibada ya Hija
Wakuu wa ufalme wa Saudi Arabia wametangaza utaratibu na kanuni za kiafya zitakazotumika katika ibada ya Hija mwaka huu, ili kuzuia kuenea ugonjwa wa COVID-19 au corona.
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Saudia, kati ya sheria zitakazotekelezwa ni kupiga marufuku au mijimuiko baina ya Mahujaji.
Mwezi Juni ufalme wa Saudi Arabia ulitangaza rasmi kwamba ibada ya Hija mwaka huu itatekelezwa na watu wachache sana, ambao ni raia na wakazi wa nchi hiyo.
Hatua hiyo ya kuwazuia Mahujaji kutoka nje ya Saudia imechukuliwa kutokana na kuendelea maambukizi ya ugonjwa wa COVID-19, ambao haujapatiwa chanjo wala dawa hadi sasa. Kwa mujibu wa taarifa, watakaotekeleza ibada ya Hija mwaka huu watakuwa takribani watu 1,000.
Aidha Mahujaji hawataruhusiwa kugusa Kaaba tukufu na watatakiwa kukaa umbali wa mita moja na nusu baina yao wakati wa ibada ya Hija, swala ya jamaa na pia wakati wa kutufu.
Kwa mujibu Kituo cha Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa Saudia, watakaoruhusiwa kuingia katika maeneo ya Hija ya Mina, Muzdalifa, na Arafat ni wale watakaokuwa na vibali maalumu vya Hija baina ya Julai 19 hadi Agosti 2. Hali kadhalika Mahujaji wote na wasimamizi watalazimika kuvaa barakoa nyakati zote ili kuzuia kuenea ugonjwa wa COVID-19.
Uamuzi wa Saudi Arabia wa kusimamisha ibada ya Hija mwaka huu, umewavunja moyo mamilioni ya Waislamu kote duniani ambao huwekeza kwa miaka mingi kwa ajili ya kutekeleza ibada hiyo na kutimiza moja ya ibada muhimu za Kiislamu.
Mwaka jana karibu Waislamu milioni mbili na nusu walitekeleza ibada ya Hija huko Saudi Arabia.
Msomi mmoja Kuwait ameibua utata katika mitandao ya kijamii baada ya kusema kuwa hatua ya kupunguzwa idadi ya Mahujaji mwaka huu itaufanya Msikiti Mtakatifu wa Makka, Al Masjid al Haram, kuonekana kama jumba la makumbusho.
Hakim al-Mutairi, mhadhiri wa Tafsiri ya Qur’ani Tukufu na Hadithi katika Chuo Kikuu cha Kuwait amekasirishwa na uamuzi wa Saudia wa kuwazuia Mahujaji kutoka nje ya Saudia kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu. IQNA.